KATIKA safu hii wiki iliyopita, tulitaka vyama vya CCM na CUF virudi mezani ili kukamilisha mchakato wa utekelezaji wa muafaka uliofikiwa baada ya miezi 14 ya majadiliano.
Lakini wakati tukihimiza hilo, tunasikitika kuona wanatokea watu wanatoa kauli zinazodisha malumbano na kuchochea chuki na uhasama dhidi ya viongozi wa CUF.
Hawa si wengine, bali ni viongozi waandamizi wa Umoja wa Vijana wa CCM (UV-CCM) na kitengo cha propaganda cha chama hicho.
Kila mmoja anajua kwamba Zanzibar kuna tatizo kubwa la kisiasa. Kama tunataka kutazama mambo kwa maslahi ya taifa, basi hakuna anayebisha.
Na hilo ndilo lililomsukuma Rais Jakaya Kikwete kumaliza tatizo alipoahidi kutafuta njia ya “kuupatia ufumbuzi wa kudumu mpasuko wa Zanzibar.”
Ahadi hiyo ilihalalisha kuanza mchakato wa majadiliano. Ni wazi CCM na CUF vimeshaafikiana, isipokuwa, tofauti zimekuja katika namna ya kutekeleza yale yaliyokubaliwa.
Katika hali kama hiyo, hatudhani kama ni busara kutokea Watanzania, tena viongozi wa juu wa CCM, wakathubutu kutoa kauli za kejeli, chuki na uhasama, dhidi ya CUF na rais kwa ujumla.
Kusema kwamba CCM kukubali kukaa mezani na CUF ni fadhila tu kwa chama cha upinzani na kwamba Rais Kikwete hana uwezo wa kumaliza mgogoro huo bila ya kushirikisha vikao vya chama chake, ni dharau kwake na kubeza kile anachokisimamia.
Rais anayo mamlaka tena makubwa, hasa ukizingatia kwamba alipotoa ahadi ile aliitoa kama kiongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Baadaye amekuja kuvikwa na uenyekiti wa taifa wa chama chake. Hayo ni mamlaka.
Anajua vizuri sababu ya kuahidi alichoahidi. Anajitambuwa kwamba kuwa kwake kiongozi wa ngazi ya juu nchini kwa muda mrefu kumempatia uzoefu wa kutosha wa kuujua mgogoro wa Zanzibar na athari zake.
Tukubaliane kuwa hali ya kuaminiana, japo kwa kiwango kidogo, iliyokuwepo kwa Kamati mbili za mazungumzo, imetoweka na msimamo wa CUF kutotaka tena kukaa na CCM, ni ushahidi tosha kwamba bado Zanzibar inasumbuliwa na mgogoro na lazima umalizwe.
Sawa, hawawezi kukaa tena na CCM, lakini na umma hauwezi kuendelea kuona nchi inarudi katika machafuko kama ilivyokuwa huko nyuma. Tunataka wote wanaohusika kuheshimu matakwa ya wananchi na muafaka uheshimiwe na kusainiwa haraka iwezekanavyo.
Katika hili, hatuoni njia ya kupita, isipokuwa Rais Kikwete kuchukuwa nafasi yake kama kiongozi mkuu wa taifa, kuelekeza na kuagiza cha kufanywa kwa maslahi ya taifa. Lazima tuondoke tulipo na twendeni mbele!


